ads

Monday 26 May 2014

SHAIRI;NANI KESHAMWONA NGUVA




Nasikia simulizi,kuhusu huyu kiumbe,
Leo sina usingizi,kanifanya nimuimbe,
Japo nalalia ngozi,nimetoa siri kumbe,
Nani kamwona nguva,aseme nami nimwone.

Nasikia kama mtu,yasemwa alivyo juu,
Samaki ama ni mtu,ama ni hisia tuu,
Kama kula wala mtu,mie nasikia tuu,
Nani kamuona nguva,aseme nikamuone.

Anaishi baharini,ama aishi ziwani,
Huyo yupo bara gani,ama yumo fikirani,
Anafanana na nani,nielezeni jamani,
Nani kamuona nguva,aseme nikamuone.

Kama yupo makumbusho,kama kiumbe adimu,
Sitaki tena michosho,nijibuni humuhumu,
Roho zenu za korosho,nguva mnamhukumu,
Nani kamuona nguva,aseme nikamuone.

Kama una picha yake,iweke nami nione,
Nijue makazi yake,niende nikamuone,
Nitatunza picha yake,wanangu wakaione,
Nani kamuona nguva,aseme nikamuone.

Kama hayupo semeni,nijue kama mazombi,
Nijue ukweli nini,naomba wala sigombi,
Nilitoe akilini,saidia langu ombi, 
Nani kamuona nguva,aseme nikamuone.

NGUVA YUKO BARA GANI,
AMENIFANYA NIGHANI

0 comments:

Post a Comment