ads

Tuesday 19 May 2015

JINSI YA KUSHINDA KINYONGO

KIKWAZO
Unashindwa kusahau mambo mabaya ambayo mwenzi wako alisema au kutenda; maneno yake makali na matendo ya kutojali yamebaki akilini mwako. Hivyo, badala ya kuwa na upendo umekuwa na kinyongo. Inaonekana kwamba huwezi kufanya lolote ila tu kuvumilia ndoa isiyo na furaha. Hilo pia linafanya uwe na kinyongo na mwenzi wako.
Uwe na hakika kwamba unaweza kurekebisha hali hii. Hata hivyo, kwanza chunguza mambo machache kuhusu kinyongo.

UNACHOPASWA KUJUA

Mume na mke wakiwa kwenye baiskeli iliyozuiwa na nanga
Kuweka kingyongo husababisha kikwazo kinachozuia ndoa yako kusonga mbele
Kinyongo kinaweza kuharibu ndoa. Kwa nini? Kwa sababu kinadhoofisha sifa ambazo ni msingi wa ndoa, kama vile upendo, uaminifu, na ushikamanifu. Hivyo basi, kinyongo si kisababishi cha matatizo ya ndoa, bali kinyongo nitatizo la ndoa. Kwa kufaa Biblia hutushauri tuondolee mbali “uchungu wote wenye uovu.”—Waefeso 4:31.
Ukiwa na kinyongo, unajiumiza mwenyewe. Kuweka kinyongo ni kama kujipiga kofi na kutarajia mtumwingine ahisi uchungu. “Huenda mshiriki wa familia ambaye una kinyongo naye anahisi vizuri, anafurahia maisha, na labda hasumbuliwi na hali hiyo,” akaandika Mark Sichel katika kitabu chake Healing From Family Rifts. Somo ni nini? “Kinyongo kinakuumiza kuliko kinavyomuumiza mtu uliyemwekea kinyongo,” anasema Sichel.
Kuweka kinyongo ni kama kujipiga kofi na kutarajia mtu mwingine ahisi uchungu
Wewe ndiye unayeamua kuwa na kinyongo. Watu fulani hawaamini hivyo. Wanasema, ‘Mwenzi wangu ndiye aliyefanya niwe na kinyongo.’ Tatizo ni kwamba mawazo kama hayo yanakazia jambo ambalo haliwezi kudhibitiwa, yaani, matendo ya mtu mwingine. Biblia inatoa suluhisho. Inasema hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe.”(Wagalatia 6:4) Hatuwezi kudhibiti maneno au matendo ya mtu mwingine, lakini tunaweza kuamua jinsi tutakavyotenda. Kuweka kinyongo si suluhisho.

 
UNACHOWEZA KUFANYA

Chukua hatua. Ni rahisi kumlaumu mwenzi wako. Lakini kumbuka, wewe ndiye unayeamua kuwa na kinyongo. Ndivyo ilivyo pia na kusamehe. Unaweza kufuata himizo hili la Biblia: “Jua lisitue [u]kiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Ukiwa tayari kusamehe utafanikiwa kutatua matatizo yako ya ndoa kwa njia ya utulivu.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:13.
Jichunguze kwa unyoofu. Biblia inasema kuna watu wenye “hasira” na wenye “mwelekeo wa ghadhabu.” (Methali 29:22) Je, wewe uko hivyo? Jiulize hivi: ‘Je, nina uchungu moyoni? Je, mimi hukasirika haraka? Je, mimi hukasirishwa na mambo madogo-madogo?’ Biblia inasema kwamba “anayeendelea kuongea juu ya jambo anawatenganisha watu wanaofahamiana.” (Methali 17:9; Mhubiri 7:9) Hilo linaweza pia kutokea katika ndoa. Basi, kama una mwelekeo wa kuweka kinyongo, jiulize, ‘Je, ninaweza kuwa mwenye subira zaidi kumwelekea mwenzi wangu?’—Kanuni ya Biblia: 1 Petro 4:8.
Amua jambo muhimu zaidi. Biblia inasema kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:7) Si lazima uzungumzie kila kosa; wakati mwingine unaweza ‘kusema moyoni mwako, ukiwa kitandani mwako, na kunyamaza.’ (Zaburi 4:4Unapohitaji kuzungumzia tatizo fulani, subiri mpaka hasira yako ishuke. Mke anayeitwa Beatriz anasema: “Ninapokasirika, mimi hujitahidi kutulia kwanza. Hatimaye, mimi huona kwamba halikuwa tatizo kubwa, na inakuwa rahisi kwangu kuzungumza kwa heshima.”—Kanuni ya Biblia: Methali 19:11.
Elewa maana ya “kusamehe.” Katika Biblia, wakati mwingine neno “kusamehe” hutafsiriwa kutokana na neno la awali linalomaanisha kuachilia kitu fulani. Kwa hiyo, kusamehe hakumaanishi kupuuza kosa kana kwamba halikutokea; kunamaanisha kuachilia kosa. Kwa sababu unatambua kwamba kuweka kinyongo kunaweza kukudhuru kiafya na kuvuruga ndoa yako hata kuliko kosa lenyewe.

0 comments:

Post a Comment