ads

Sunday 7 May 2017

SHAIRI; NENO LANGU KWAO.



Uchungu wake mzazi,mlenzi ama rafiki,
Moyo unakufa ganzi, ndugu anapofariki,
Imekuwa  wanafunzi, na kuleta taharuki,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Zile ndoto zake mama,ama baba kwa mwanaye,
Jana zimeshasimama,na kuisha hatimaye,
Ni ajali siyo homa, leo hii hawanaye,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Vimezimishwa vipawa,walivyobeba watoto,
Bila ya kugusa dawa,imekuwa kama ndoto,
Ni kama imezinduwa,ShauriTanga na moto,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Walimu waliopotea,na wale waliowapenda,
Dereva katangulia,kaenda na alowapenda,
Shule hakujatulia,myoyo yabaki kudunda,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Pole kwa wanafunzi, mloguswa na hili,
Pole kwa mama wazazi,muweza kustahimili,
Pole pia kwa walezi, leo mwaona miili,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Pole kwa watanzania,nchi imetikisika,
Hili kulishuhudia,myoyo inatetemeka,
Arusha yote walia,wanetu kuwakumbuka,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Naandika kama baba, kaka na mwalimu wenu,
Kwenu darasa la saba,mlofiwa na wenzenu,
Tuwaombee kwa baba,awapokee wenzenu,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Na wale wadogo zao,waliwaacha shuleni,
Pole na ziende kwao, nguvu mtiwe yoyoni,
Msiwaze yale yasiyo, wamekufa ajalini,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Laweza mkuta yeyote, si fukara si tajiri,
Hivyo tuyafute yote, kudhani yasiyojiri,
Na tuwafariji wote, hima bila kusubiri,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Pia niwaase jambo, kwa watumao zao picha,
Hayafai hayo mambo, ni watu siyo mchicha,
Ama tuzishike fimbo, ndipo mtaja zificha,
Neno langu dogo kwao,poleni kwa hili gumu.

Kaditama nasimama,poleni kwa mama zao,
Ninaumia mtima,kuwazia baba zao,
Naingiwa na huruma,juu ya walimu wao,
Mwisho nabaki kusema,wapo naMungu wao.



0 comments:

Post a Comment