ads

Sunday, 24 April 2016

NANI HASA ALISTAHILI UFALME WA RHYMES MWAKA 2004?


 Na.Steven Mwakyusa(Mtu Makini)
Shindano la kumsaka mfalme wa Rhymes katika bongo flava ni moja ya shindano lililopata msisimko mkubwa kwa kipindi hicho, hii inawezekana ilitokana na kukutanishwa manguli wa muziki kwa kipindi hicho hali iliyopelekea uamuzi wa nani ashinde kuwa mgumu wa walio wengi!
Shindano liliwakutanisha Jay moe(kama unataka demu), Afande Sele(Darubini kali), Prof J(), Inspector Haroun (Bye Bye), Solo Thang(Mtazamo), Madee(Kazi yake Mola), MwanaFA(Unanitega), Mandojo na Domokaya(Nikupe nini), Soggy Dogy(Kulwa na Doto) na Dully Sykes, ila Dully alijitoa siku chache kabla ya shindano!!
Shindano liliandaliwa na Global Publisher chini ya E. Shigongo na zawadi kwa mshindi wa kwanza lilikuwa gari, japo sikumbuki ni gari ya aina gani!!
Shindano lilifanyika usiku wa tarehe 27 June(siku ya ijumaa), na hatimaye Afande Sele kutawazwa kama mshindi na kuwa mfalme wa rhymes, huku ushindi wa pili ukienda kwa Inspector Haroun na ushindi wa 3 wakichukua akina Mandojo na Domokaya!
Ushindi huu ulipingwa na watu wengi kuanzia watu wa kawaida mpaka wasanii wenyewe!!
Haikupita muda Solo Thang aliandika wimbo akipinga kile kinachoitwa kupanga mshindi, namnukuu "wengine wananirubuni eti nashindania gari, kumbe washapanga wampe nani toka awali, sitarudia kosa hata zawadi waweke meli, wanipe ghorofa mbili wanikabidhi na sheli"
Solo Thang akuishia hapo, katika wimbo wa Traveller anasikika tena akisema "Mi siyo mfalme njozi mi siyo mgambo sele"
Fid Q naye katika Mwanza Mwanza aliendelea kuthibitisha kutokukubalika kwa ufalme wa Afande, namnukuu "Mfalme wa Rhymes ambaye Soggy Doggy hamtaki, anamwita Kobe hawezi mzidi mbio farasi"
Madee naye alienda mbali na kudai hajawai ona mfalme ana nywele chafu!!
Sasa ni takribani miaka 12 imepita toka Afande Sele atangazwe kuwa mfalme wa rhymes na hajapata mrithi wake, mwaka 2005 shindano halikufanyika baada ya washiriki kudai maslahi zaidi huku wengine wakipinga kunakoitwa kupangwa mshindi ambaye ilisemekana alitakiwa kuwa Fid q, ambaye alishajinadi kuwa ni mfalme atakayefuatia baada ya Selemani Msindi!!
Je Afande Sele alistahili ufalme wa Rhymes? Kama hakustahili nani alipaswa kupewa hilo taji?

Saturday, 23 April 2016

HIVI ILITAKIWA MADAWATI KUWA SUALA LA DHARULA?


Na.Mwanakalamu.
Juzi nilikuwa nikiongea na rafiki yangu mmoja mbaye nilisoma naye nikiwa darasa la tatu,huyu sikuwahi kuonana naye tena wala kusikia habari zake lakini juzi alibahatika kupata namba yangu kupitia facebook.
Baada ya salamu na maswali mengi ,sijui umeoa ,una mtoto, unafanya kazi gani sijui nani sijui ana wake wawili mara yule jirani alifariki na mengine mengi akagusia ile post yangu kuhusu vipaji.
Nikakumbuka naye alikuwa na kipaji cha kuchekesha ,huyu alikuwa bingwa tulicheka hadi tukasahau kufanya zoezi la kusoma kiingereza tulilokuwa tukipewa na mwalimu tuliyekuwa tukimwita Oldonyo jina ambalo rafiki yangu yule alimpa ,likawa jina la mwalimu bila hata yeye kujua.
Nikamuuliza kama anahitaji namba za wachekeshaji wenzake, lakini akakataa akasema hiyo kazi niwaachie akina mpoki maana walijiongeza na akaniuliza kuhusu ukweli wa habari kuwa mpoki ni mtangazaji, nilipomthibitishia akakohoa kisha akaongea kwa kusikitika.
''Ameshajitengenezea njia , unadhani ni nani hatomuajiri hata kama serikali itasema watangazaji elimu yao ile shahada ya kwanza na yeye awe na cheti, tayari ni bidhaa''
Nikaona anaongea kwa huruma sana nikaamua kumtoa huko na kumuuliza vituko vya kugombana siku za kufunga shule , lakini hakuvifurahia aliguna tuu na kuongea mengi.
''Unajua Moringe ule mwaka si matokeo yetu yalifutwa kisa watu wawili wa MEMKWA walifanya mtihani kama wanafunzi wa kawaida wakaonekana kuwa wamerudia shule kitu ambacho si sahihi kwa darasa la saba''
''Mhhh poleni sana , samahani sikuwa na taarifa hiyo kaka si unajua niliondoka nikiwa mdogo''Nilongea nikiwa siamini nilichokisikia kwani nilijua mwenzangu atakuwa alifika hata sekondari kwani hakuwa mbaya kitaaluma.
''Basi nikashindwa cha kufanya nikenda kwa yule fundi selemara aliyekuwa akichehemea mguu mmoja sijui unamkumbuka?''

''Ndiyo si yule wa kwenye mapera?''
''Ndiyo nikaanza kumsaidia kazi huku najifunza na baadaye nikawa fundi kweli , halafu si uliniambia hujaoa basi kitanda cha kumtafutia mtoto itabidi nikuchongee bure si unakumbuka siku ile yale maandazi mawili uliyokuwa umepewa na mama yako kuyauza halafu ukanikopesha halafu sikukulipa mama yako naye kwa kukufundisha biashara alikuchapa nilikuhurumia ila si unajua maandazi yenyewe niilikuwa nampa Monika''
Nakikumubuka kisa hicho na kucheka.
''Unakumbuka kumbe ,we jamaa ulinikomoa na Monika mwenyewe kaolewa''
''Si nimesema nitakuchongea kitanda bure ama unanunua vya kichina laki nane? mama nasikia umefika hadi chuo kikuu''
''Chuo wapi umasikini tuu''Namjibu kinyonge kwani anaonekana kama anawaona watu waliofika chuo kikuu ni matajiri.
''Baada ya kumaliza mafunzo na kuwa fundi kamili nikaenda VETA kusomea nipate cheti, aisee kumbe veta wanafundisha kutengeneza hadi samani zile tunazoziona kwenye televisheni sema tuu kule nyumbani haujafika umeme''
''Kwa hiyo umeshatoboa baada ya kutoka VETA''
''Hakuna cha kutoboa wala kuziba nina ujuzi na vifaa nilivyoachiwa na yule fundi wa kule nyumbani si alihama pale kijijini''
''Dah!''Nakosa cha kuzungumza.
''Basi nawachongea watu meza ,fremu za madirisha na milango, milango,vitanda kwa hela za maji wakati mwingine hata hazitoshi kunua chumvi'
Hata tenda ya kurekebisha paa la shule tuliikosa likaja kampuni wakaja kurekebisha wakati siku za nyuma tuliitwa kama wanakijiji tuu na mwisho wa siku tuapikiwa tuu ugali tunakula na kusamehewa kwenda kufyatua tofari za shule ya kata siku mbili''
''Moringe usione hii nchi wanasema inakua kiuchumi, nyie wasomi mnaamini hivyo lakini we na usomi wako huamini kama tungepewa elimu ya kuwa na vikundi ambapo tukakopeshwa vifaa vya kisasa leo hii wangehangaika madawati hadi kulifanya suala la dharula eti wanajeshi wakatengeneze, si matusi hayo?
Kama hujabadilika ile tabia yako ya kujiongeza , najua hujabadilika juzi umeandika mengi sana mazuri kuhusu vipaji umenigusa ukanifanya niingie mtandaoni kusoma mengi tuu ya kujiongeza ufanikiwe, ile komenti yako kwenmye post ya Shigongo imeniaminisha kuwa wewe ni Moringe halisi mzee wako hakukosea kukupa hili jina''.
Unasinzia eeh, lala bhana ila naamini suala la madawati halikuwa la dharula na hata tusilalamike sana.
''Sijala'' Najibu nikiwa natafakari mengi juu ya maneno yake.
''Mbona kimya basi nipe jibu suala la madawati ni dharula?''
''Hapana''
''Je ,utanunua kitanda cha supamarket ama utaniagiza nikuletee?''
''Hata cha kwako tutaweka supermarket kaka''Namjibu kwa hamasa.
''Kweli?''
''Ndiyo''
''Nasubir''
.........simu ikakakata nikampigia akawa hapatikani.

Share ifike mbali tupate jibu kama kweli suala la madawati lilikuwa la dharula.

UKOLONI ,UJAMAA , SHULE ZA KATA NA UJANJA WA KISASA


Na.Mwanakalamu
Imekuwa fasheni katika miaka ya karibuni watu kukosoana kwa asili zao, hali zao za maisha, rangi , maumbile yao na hata aina ya elimu waliyonayo ama waipatayo.
Si tatizo watu kukosoana , bali wakosoane kwa hoja na hoja haziji kwa hulka, mihemko ama mahaba na jambo jadiliwa bali hoja huja kwa ujuzi na maarifa ambavyo ni zao la elimu.
Elimu ni nini?
Ukitaka kujua maana ya neno elimu unaweza ukaja na majimbu mbalimbali kichwani mwako ama kwenye vichwa vya watakao kupa hiyo maana.
Kwa uelewa wangu elimu ni ujuzi ama stadi ambazo mtu ama kiumbe hujifunza (kwa hiari ama lazima) ama hufunzwa ili kukabiliana na mazingira.
Viumbe hukabiliana na mazingira ili kuweza kuishi na kutengeneza maisha bora ya vizazi tarajiwa.
Kwa binadamu elimu hutolewa /hupatikana kwa njia kuu mbili ile iliyorasmi na isiyo rasmi.Mifumo isiyorasmi ilianza tangu zama za ujima ambapo kupitia elimu moto ukapatikana, watu wakafuga, wakawinda na kufanya mengi ambayo yamekuja kusaidia vizazi vilivyofuata na mifumo rasmi kwa barani Afrika ililetwa kipindi bara hili lilipoanza kushirikiana na jamii za mabara mengine kama Asia na Ulaya huku mashirika ya dini ya kiisalam na kikristo.
Elimu hii ya mfumo rasmi ambako kuna mitaala iliyoandikwa ndiyo iliyoleta mbadiliko makubwa katika jamii nyingi za kiafrika.Hapo ndipo mgawanyo wa kazi na matabaka yakatengenezwa na kuimarishwa badala ya matabaka kuwa katika nyanja za uchumi na kisiasa pekee elimu hii iliongeza matabaka ya waliosoma na wasiosoma kisha hata uchumi na siasa ukaanza kuingiliwa na matabaka ya elimu.
Kwa Tanganyika, elimu ya mfumo rasmi iliyoletwa na watangulizi wa wakoloni ikatumika kipindi cha ukoloni hadi wakati wa azimio la Arusha.Elimu ile iliyolenga kutoa ujuzi kidogo na kuandaa watumishi wa kuwatumikiwa wakoloni na kuimarisha dola yao ,ilifanyiwa mageuzi kadhaa ambayo bado madoa yake ni ngumu kufutika.
Baada ya azimio la Arusha ikaonekana misingi bora ya kuifanya elimu kweli ni njia ya kuifanya jamii iweze kukabili mazingira(kuyafanya mazingira kuwa mahali pa kuishi na kupata mahitaji kiurahisi/maendeleo).
Ugunduzi ulizingatiwa ,uzalendo na utamaduni pia , lakini baada ya miaka kadhaa pale tulioingia kwenye ile mipango ya kimaendeleo ya kibepari (SAP na mingine kama hii) hapo tukapoteza lengo na kujikuta tukitumbukia kwenye ile elimu tuliyoikataa wakati tunaleta azimio la Arusha.
Mitaala ikaanza kubadilishwa na wanasiasa walivyojisikia, shule tena haikuwa mahali pa kupata uzalendo bali kuwagawanya watu katika matabaka ya waliosoma na wasiosoma.Kuwa na elimu ikawa ni kufika sekondari ama chuo kikuu na si shule ya msingi na VETA.
Baadaye ziakaanzishwa shule zilizokuwa na mlengo wa kijamaa (shule za kata) na zikaanza kufanya kazi ya kibepari.
Hapo ndipo ujanja wa kisasa ulipoanza, tuliobahatika kusoma shule hizo tukakosa ujanja, usichangie sehemu utaambiwa ulisoma shule za kata, hamna kitu ni kayumba nyie hamjui kiingereza sayansi hamuijui wazee wa zero na mengine mengi hapo ujanja ni kutosoma shule za kata wakijua umesoma huko una hatari.
Walioanzisha shule za kata na walioanza kutoa mawazo haya ni wale ambao ama walipata elimu ya kikoloni ama ya kijamaa sasa tumlaumu nani aliyesoma shule za kata ama aliyeanzisha shule za kata kwa kujua ama kutojua ili kuleta matabaka.Shule zilizoitwa za vipaji maalum hazikutosha kupokea wanafunzi wote walifahulu kukahitajika mbadala lakini hawa wasomi wa zamani wakatuletea mbadala usiokamilika na madaraja yakaongezeka.
Nitawaambia wanangu kuwa sikutoka kapa kusoma shule za kata japo tulionekana masikini na wasio na akili nilipata ujuzi ambao ulinifanya nikaishi maisha bora pengine kuwazidi wale waliojiona bora, shule za kata ndizo zilizokuwa daraja nikafika kidato cha tano na chuo kikuu ambako nikakutana na wajanja wa shule za matajiri wanaoongea kiingereza kama malkia lakini wana ujuzi sawa , zaidi ama kidogo kuliko ujuzi nilionao.
Hao ndio niliowahi kuwapa akili ya kupika wali na chai na kukifanya chakula cha jioni nilipowakuta wakilia hawana mboga huku wana mchele na sukari ndani kifupi walishindwa kupambana na mazingira licha ya ujanja wao.

Share ifike kwa kizazi kijacho

Thursday, 21 April 2016

ANAITWA ALLY SALEH KIBA





Na.Mwanakalamu

Alikiba ama King kiba alianza harakati za muziki kitambo kidogo tofauti na wanamuziki wengi wanaotamba kwa muda huu.Mwanamuziki huyu anayetamba na nyimbo kadhaa mjini akiwa chini ya usimamizi wa Rockstar 4000 hajaanza leo kutoa hit baada ya hit na tangu 2006 alionekana kuteka masikio na akili za watu wengi na mwaka uliofuata alikuja na albam iliyokuja kuvunja na kujiwekea rekodi ya mauzo.Ingawa mitandao ya kijamii haikuwa na nguvu sana katika kutangaza nyimbo na kazi za wanamuziki mwanamuziki huyu alifanikiwa kuwateka wengi kuwa na albam  yake iliyokuwa na nyimbo kali ambazo hazikuhitaji watu kusubiri zaidi kumkubali mwanamuziki huyu.

Thursday, 14 April 2016

GAMBOSHI KIJIJI KINACHOBEBA DHANA NGUMU KUAMINIKA

 Wakazi wa kijiji cha Gamboshi
Wengi tumekuwa tukisikia habari nyingi kuhusu kijiji cha Gamboshi kilichopo wilayani Bariadi.Kijiji hichi kimekuwa kikihusishwa na uchawi na ushirikina huku ikisemwa kuwa kina maajabu mengi sana.Kwa wale waliokuwa wakisikiliza  kipindi cha sitosahau kupitia Redio Free Afrika kipindi kile watakuwa wamewahi kusikia habari kuhusu maajabu ya kijiji hicho, mwandishi nguli wa hadithi nchini Eric Shigongo aliwahi kuandika hadithi akitumia jina la kijiji hicho.
Kuna wale ambao walikuwa wakihisi kuwa jina hilo ni la kubuni na hakuna kijiji kama hicho.
Nimekuwekea makala iliyowahi kuwekwa kwenye gazeti la mwananchi miaka kadhaa iliyopita . isome hapa chini;

Kijiji hicho ambacho ni nadra sana kutembelewa, kimepata umaaurufu mkubwa ndani na nje ya nchi kikielezwa kuwa ni kitovu cha uchawi na wachawi wanaoweza kufanya miujuza, hali ambayo imekifanya kijiji hicho kupitwa na mkondo wa kimaendeleo.
“Sisi ni wakulima wakarimu wa pamba, mahindi na mpunga. Yote mnayoyasikia kwamba sisi ni magwiji wa uchawi ni uvumi uliotiwa chumvi nyingi. Tunamwomba Rais wetu kwa kushirikiana na Mbunge wetu, Andrew Chenge watusadie kulisafisha jina letu,”alisihi Zephania Maduhu, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Gamboshi.

Maduhu pamoja na wanakijiji wenzake walidai kuwa, hofu iliyoenezwa ndani na nje ya nchi kuhusua uchawi uliovuka mipaka wa Kijiji cha Gamboshi umesababisha madhara makubwa kwa kijiji chao kiasi chakutengwa na jamii yote ya Watanzania.
 “Hakuna aliyetembelea kijiji hiki kwa miaka mingi sana. Hata sisi tunapotoka nje ya kijiji, wengi hawataki kutusogelea wakiamini tutawadhuru, ” alisema Musa Deus (26), mmoja wa wakulima walionufaika kilimo cha mkataba kijijini Gamboshi.

Kwa mujibu wa Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho, tangu Uhuru mwaka 1961, hakuna kiongozi yoyote wakitaifa aliyewahi kukanyaga kijijini hapo.

Anaongeza kuwa mtu wa pekee aliyewahi kuzuru kijijini hapo ni mbunge wa Bariadi Mashariki, Andrew Chenge, aliyefika kijijini hapo mwaka 2010, wakati akifanya kampeni za ubunge.

“Tume ya Katiba ilitupita, mwenge wa Uhuru nao haujawahi kupita hapa. Tuko kisiwani mbali na Watanzania wengine,” anasema Maduhu.

Kikiwa mafichoni kabisa, kiasi cha kilometa 44 kutoka mjini Bariadi, Kijiji cha Gamboshi si rafiki wa watu wa Kanda ya Ziwa kama ambavyo Mwananchi Jumapili ilibaini katika utafiti wake wa muda mrefu.

Mijini na vijijini, kumekwepo na ubishani mkali kuhusu ni mkoa gani unaokimiliki kijiji hicho, ambacho baadhi ya wakazi wake wanadai kuwa miongoni mwa vioja vyake ni mauzauza yanayoweza kuifanya Gamboshi ionekane kama Jiji la New York, Marekani au London, Uingereza wakati wa usiku.

Pamoja na umaarufu wake, bado uwepo wa Gamboshi umekuwa ni kitendawili kikubwa kwa jamii ya Wasukuma kutoka mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Simiyu.

Mbali na ubishani mkali kuhusu kuhusu mahali hasa kilipo kijiji hicho cha miujiza, wengi wamekuwa wakidai wakazi wake siyo jamii ya Kisukuma.

Wakazi wa Shinyanga wanadai kuwa Gamboshi iko wilayani Magu, Mkoa wa Mwanza, wakati wale Mwanza wakidai kuwa iko mkoani Shinyanga.

Kwa mujibu wa Maduhu, Gamboshi iko katika Wilaya Bariadi, karibu na mpaka unaotenganisha na Wilaya ya Magu iliyoko mkoani Mwanza.

“Tunaomba sana ndugu mwandishi, waambie Watanzania kuwa mengi wanayoyasikia kuhusu Gamboshi siyo kweli kabisa. Tunawakaribisha wote waje hapa kufanya biashara na sisi, waoleane na vijana wa Gamboshi kama wafanyavyo katika vijiji vingine. Sisi ni binadamu wema,” anasema mkazi wa kijiji hicho, Malimi Kidimi ambaye ni mkulima.

Ofisa Mkaguzi kutoka Bodi ya Pamba (TCB), Ramadhani Dissa, anaielezea Gamboshi kuwa ni moja ya vijiji vilivyouza pamba nyingi msimu huu.

Anasema kuwa Wilaya ya Bariadi, kilipo kijiji hicho, imeweza kuuza robo ya pamba yote iliyouzwa nchi nzima hadi kufikia katikati ya Oktoba mwaka huu.

Kwa mujibu wa Dissa ni maofisa wa bodi ya pamba tu ndiyo wanaofika kijijini hapo na kwamba siyo wananchi tu wanaogopa kufika hapo, bali hata baadhi ya kampuni za ununuzi wa pamba.

“Kampuni ya Billlchard, moja ya mawakala wa kilimo cha mkatabaka alishindwa kutuletea mbolea hapa, badala yake akaenda kuibwaga katika Kituo cha Polisi Bariadi kwa kile ambacho wafanyakazi wake walidai ni kuhofia usalama wao,”anasema Maduhu.

“Pigo tulilopata kutokana sifa mbaya tuliyobambikiziwa haisemeki na madhara makubwa tunayapata kutokana na kutengwa na jamii. Wanakijiji wa Gamboshi ni masikini kwa sababu mkondo wa maendeleo na mageuzi umepata mbali sana nao,” anasisitiza Maduhu.

Chanzo cha hofu
Akifafanua kiini cha chuki na hofu hiyo, Maduhu alidai kuwa hapo zamani ilitokea kijana mmoja kutoka kijiji jirani cha Ngasamwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na msichana mzaliwa wa Gamboshi.
“Siku moja kijana huyo alikuja kijijini hapa akimsandikiza mpenzi wake, kisha kushindwa kurudi kijijini mwake,” anasimulia Maduhu akiongeza, “Juhudi za kumsaka kijina huyo hazikiweza kuzaa matunda, hadi aliponekana kichakani baada ya siku saba, huku ngozi yake imebadilika na kuwa nyeupe.”

Anaeleza kuwa alipouliza alifikaje kichakani hapo, kijana huyo alijibu kuwa ameteremshwa na ndege kutoka Ulaya na baada ya hapo kijana huyo alirukwa na akili na kushindwa kuuongea.

“Ilibidi achukuliwe na kupelekwa kutibiwa na waganga wa jadi na akapona baada ya matibabu ya zaidi ya mwezi mmoja,” anasema Maduhu akieleza kuwa kisa hicho kilitiwa chumvi nyingi licha ya kuwa na ukweli kiasi.

Anasema kuwa, tangu siku hiyo Gamboshi ikatangaziwa uadui na vijiji vingine kiasi cha kukifanya kuogopwa na kuchukiwa.

“Uvumi kama Gamboshi inaweza kuonekana kama Ulaya au Marekani ulianzia hapo na umendelea kurudifiwa na kukikifanyakijiji hiki kiitwe jiji la maajabu,” alidai Maduhu.

Sisi ni wasafi
Mkazi mwingine wa kijiji hicho, Malimi Kidima anasema kuwa wana Gamboshi wangeweza kuitangazia dunia kuwa wao ni wasafi lakini, kwa miaka mingi wamekosa jinsi ya kuifanya sauti yao isikike.

Hakuna redio wala Luninga
“Redio ndiyo njia ya pekee inayotufanya sisi tuwe karibu na dunia, Hakuna mwenye luninga hapa kwa sababu hakuna umeme. Tunasoma magezeti kupitia vichwa vya habari vinavyosomwa kila siku redioni,” anasema Kidima.

Mkazi wa Lamadi, wilayani Magu, Anthony Mashimba alidai: “Gamboshi ni jiji la ‘masupastaa’ wa uchawi hawatakuachia ufike huko.”

Tofauti na wengine, Mkurugenzi wa Bodi ya Pamba ya Kanda ya Ziwa, Jones Bwahama alitoa uhakika na kusema Gamboshi imekuwa ikifikiwa mara kwa mara.
Mauza mauza ya kwanza
Kutoka Bariadi mjini ni lazima upitie kijiji cha Ngulyati kiasi cha kilometa 30 Mashariki ya Bariadi katika barabara itokayo Bariadi kwenda Magu.

Hakuna kibao kinachotambulisha Kijiji cha Gamboshi mwanzoni mwa barabara ya vumbi inayoelekea Gamboshi kuanzia Ngulyati.

Watu walikuwa wengi katika kilometa 5 za awali kuelekea Gamboshi, lakini idadi ikazidi kupunguia kwa namna tulivyozidi kukikaribia kijiji hicho.

Barabara ilikuwa tupu hadi kilometa tano kukufikia Gamboshi hali ambayo ilianzisha hofu mpya hata kwa mwandishi wa makala haya.

Nyumba nzuri mfano wa shule za kisasa za ‘English Medium’ ilionekana kuvutia macho kilometa chache kabla ya kukifikia Kijiji cha Gamboshi.

“Ile ni shule ya Serikali au ya mtu binafsi,” aliuliza mmoja wa watu tuliokuwa nao katika safari hiyo baada ya macho yake kuishuhudia kwa mbali.
Lakini kwa mshango dereva alisema: “Hakuna shule yoyote ule ni mlima tu wa mawe mengi.”

Ilioneka dhahiri kuwa ni nyumba, lakini hata tulipopiga picha kwa kamera niliyokuwa nayo, picha ilionesha kuwa hakuna nyumba yeyote.

Baada ya mwendo, Kijiji cha Gamboshi kikaanza kuonekana kikipambwa na miti ya Jakaranda yenye maua mekundu, kiliioenekana ni kijiji kizuri, chenye nyumba chache na hali yake kunogeshwa na ubaridi uliotokana na miti mirefu iliyopandwa kuzunguka nyumba chache zilizokuwepo.

Habari hii imenukuliwa kwenye tovuti ya Mwananchi kupitia gazeti lake la Mwananchi Jumapili, kama ilivyoandikwa na mwandishi Miguel Suleyman.



WAJUE MABINGWA WA CHORUS KWENYE BONGO FLEVA


Wajue mabingwa wa chorus wa muda wote katika bongo fleva!!

Na.Steven Mwakyusa.
 Kuna wasanii wengi ambao wamekuwa wakifanya vizuri katika muziki wetu, iwe katika nyimbo zao ama kwa kushirikishwa..

Msanii anapokuwa mzuri katika nyimbo zake mara nyingi anakuwa kimbilio la wasanii wengine kutaka kufanya naye kazi, ukiachilia mbali Hiphop ambayo imekuwa ikihitaji watu wenye uwezo katika viitikio, wasanii ambao wamekuwa na uwezo mkubwa wa kucheza na viitikio wamekuwa kimbilio hata kwa wasanii wenzao ambayo wanafanya muziki wa aina moja!

Hii ni rekodi yao kuanzia kuanzia miaka ya 2000 mpaka sasa!!

1. Dully Sykes/Handsome/Mr Misifa

2. Juma Nature/Sir Nature/Kiroboto

3. Q chief/Q chilla/Savimbi

4. Lady Jd/Komando Jide

5. Alikiba/KingKiba

6. Belle 9

7. TID/Mnyama

8. G nako

9. JUX

10. Ferouz

NB; Wapo wengi pia waliofanya na wanaofanya chorus nzuri kama akina Barnaba, Banana Zorro,Linah, Benpol na Rama D lakini hao 10 ndiyo walioweza kuimba chorus nyingi na kuzifanya nyimbo husika ziwe hits!!

OMMY DIMPOZ? SIAMINI

Na.Mwanakalamu
Jina Ommy Dimpoz likitajwa nchini kila mtu atajiwa na taswira ya mtu mmoja ambaye aliikamata Afrika mashariki kwa nyimbo zake kali ambazo zilikuwa zikienda kuikamata Afrika nzima.Mtu ambaye ndiye alitoa 'hit' baada ya 'hit' aliyetoa Nai nai , baadaye, Me and you, Tupogo, Wanjera na Ndagushima.
Utamkumbuka Ommy aliyekuwa akionekana mshindani wa Diamond Plutnumz kwenye muziki, Ommy ambaye wengi tunaamini alitufanya tukamfahamu binti mmoja ambaye leo hii ni moto wa kuotea mbali barani Afrika baada ya kumshirikisha kwenye Me and you , Vanessa Mdee.
Naam lakini wakati taswira hiyo ikikujia akilini mwako kuna taswira nyingine itajiingiza akilini mwako taswira yenye maswali mengi kuwa yupo wapi huyu mkali?
Utajijibu mwenyewe kuwa yupo bongo na huwa anaenda Nairobi na Marekani anafanya nini?
Pia utajijibu mwenyewe kuwa ni mwanamuziki ambaye ametoa wimbo uitwao Achia Body ambao video yake ni aibu kuiangalia ukiwa na wenzako hasa kama ni mwanaume , utajilazimisha kutafuta funguo mfukoni, video ambayo ina mashairi mepesi ambayo angeimba mtu kama Nuh Mziwanda basi wimbo wake ungeishia kutambulishwa kwenye stesheni za redio na televisheni na kuwekwa kapuni lakini kwa kuwa ni Ommy wengi wakhisi kuna kitu cha ziada kwenye wimbo huo na kujaribu kukitafuta na kuufanya wimbo huo kushika chati kwa muda fulani kabla ya kuzimwa taratibu.
Ni Ommy huyu huyu ambaye aliimba na J Martins ambaye leo hii hasikiki kama ni mwanamuziki , show za peke yake ama zile pamoja kubwa hazisikiki tena.
Ameamua nini ama ndo ameridhika na kuwa kama Sam wa Ukweli ama Marlow?
Anataka kupumzika kama Ally kiba?
Ameamua kufanya biashara nyingine?
Majibu anayo yeye , ila kwangu nilianza kuhisi kupotea kwa mkali huyu pale tuu alipotoa Tupogo ambapo nilijua ni nyimbo zinazotegemea zaidi nguvu ya mwanamuziki kwenye media na si ukubwa wa wimbo alipotoa ndagushima hata wanjera nikaona ni yale yale wimbo mtamu lakini hauna uwezo wa kuishi muda mrefu.
Ommy Dimpoz? Wala siamini kama ndo kaamua kupoa hivi huenda kuna mambo matamu yanakuja maana wanamuziki hawa nao wana 'timing' zao.

NYIMBO KUMI AMBAZO DIAMOND PLUTNUMZ HATOZISAHAU!


Na.Mwanakalamu
Diamond ni habari ya Afrika, ametoka kufanya matamasha ya muziki makubwa barani Ulaya na Marekani na kuteka hisia za wapenzi w muziki wake kila anapotumbuiza.
Ametoka wapi huyu Milionea ambaye kila akanyagapo panageuka dhahabu?
Mwenyewe anasema ''From Tandale to the World''.
Naam katoka Tandale ambako ''alihaso' sana kabla ya kutoboa , alianza kwenye sifuri hadi kwenye tunayoiona mia ila kwake anaweza akasema ndo kwanza yupo arobaini, nani alikuwa anajua kuwa angefika alipofika?
Naamini hayupo na kama wapo basi ni wachache sana na huenda hao wachache walikuwa wakimwombea tuu hayo ama wakiota, lakini ni kweli amefika ambapo kwa jicho na akili ya kawaida hakuna ambaye angewaza.
Alipochukua tunzo nyingi Bongo angebweteka lakini hakufanya hivyo akapiga hatua, alipotajwa kuwania tuzo za BET angejisahau lakini alikaza mwendo na hata alipochukua AFRIMA ahakusimama na hatimanye tunzo hizo zikamzoea akazibeba za kutosha na Mtv nazo zikaweka kambi kwake, lakini hajasiama leo hii kavuka mabara , anafahamika kwote huko na bado anapiga hatua.
Najua ni funzo kwako kijana na hata mzee unayeridhika , kwa kidogo tuu ukipatacho.
Kama nilivyosema awali , kijana huyu alianzia sifuri ambako ni watu wa mtaani kwake na mitaa ya jirani pekee ndip waliojua kipaji chake hadi alipofika leo , leo tutaangalia nyimbo kumi ambazo daima atakuwa akizikumbuka na kuziwekea uzito kila akizisikia.
1.KAMWAMBIE
Huu ni wimbo ambao ulitufanya wapenzi wengi wa muziki tumtazame kijana huyu kwa jicho la ziada.Ulikuwa ni wimbo wa nguvu ambao bila shaka hautosahaulika kichwani mwake kwani ndio ulimtengenezea njia nchini na hata nchi za jirani zinazotumia kiswahili.
2.MBAGALA
Kikawaida mwanamuziki hupimwa na wimbo wa pili kama kweli anakipaji ama alibahatisha wimbo wake wa kwanza.Lakini Diamond alithitisha kipaji chake kwa wapenzi wa muziki kwa kutoa wimbo huu ambao uliikamata Afrika mashariki na kumfanya atazamwe kama moja ya wasanii wakali ambao walikuwa wanakuja kuikamata Tanzania.
Wimbo huu pia ulimfungulia njia ya kimataifa kwani ulifanikiwa kuingia kwenye kuwania tunzo za muziki za Mtv licha ya kutoshinda.
Bila shaka yoyote utakuwa umebaki kwenye kumbukumbu zake daima.
3.NALIA NA MENGI
Wimbo huu ambao aliuimba na Rapa Chid Benz ulionekana kubeba hisia nyingi za maisha yake na ujumbe mzito.Nadhani historia ya maisha yake ilimsukuma kuandika wimbo huu ambao licha ya kutotamba sana redioni ulibaki kwenye 'playlist' za watu wengi wakiusikiliza ujumbe huo.
Kwa kubeba historia yake ya maisha daima wimbo huu hautosahaulika kwake.
4.MOYO WANGU
Yaap! hapa ndipo patamu, ilikuwa ni baada ya kutoka kwa Bob Junior ambako alikuwa ameshatengeneza albam nzima , lakini matatizo katika kutengeneza wimbo wa gongo la mboto yakamfanya kijana huyu kutoka Mbagala ajiongeze na kuanza kurekodi kwingine na akaanza Fishclub kwa Lamar ambaye kwa kipindi hicho alikuwa moto wa kuotea mbali.
Moyo wangu licha ya kuonekana ni wa kawaida mwanzoni ulikuja kuikamata Afrika mashariki na kuwa moja ya nyimbo bora kuwahi kutokea kutokana pia na ubunifu wake kwenye video.
Bila shaka wimbo huu ulikuwa ni mwanzo wa mabadiliko ya kimtazamo wake katika muziki na kuwa moto wa kuotea mbali.
5.NUMBER ONE
Wimbo huu unaweza ukawa ulimlipa na kumpooza mateso aliyokuwa amepitia kwani ulimpa nguvu ya kuvunja rekodi katika tunzo za muziki za Kili na kumfungulia vizuizi vingi vya kimataifa nakisha kumuweka juu.
Number one wimbo ambao huenda kila akiusikia anajikuta akicheka sana kwani ulipelekea kufanyika kitu ambacho nacho huenda hakukifikiria awali.
6.NUMBER ONE REMIX
Huu ni zao la number one ambao aliamua kufanya na Davido ambaye ni kama walicheza bonge la kete kwani Davido akajenga ngome Bongo na Diamond akatoboa.
Wimbo huu ukampa tunzo na njia zaidi za kwenda mbele kimataifa na 'koneksheni' nyingi zilianzia hapa.
Diamond Plutnumz akiusikia huu wimbo huenda akafungua jokofu na kuchukua maji ya baridi na kuyanywa maana anaweza furahi hadi akazidiwa.
7.MDOGO MDOGO
Nilipofanikiwa kuiona 'Behind scene' ya video ya wimbo huu, ilikuwa ni zaidi ya kutafuta, hapo nilimwona Diamond ni mtu wa tofauti na wa ajabu sana , licha ya jina lake na mapesa aliyokuwa nayo alikubali kupigwa na baridi kali la mji mmoja aliopo Afrika kusini ili tuu atengeneze video ya wimbo huu.Hakika yalikuwa mateso angeweza kumfanya mtu mwingine achukue uhusika wa mahali pale ambapo ilimpasa kuteseka ,lakini aliamua kuifanya kazi kwa ukomavu wa hali ya juu na hatimaye wimbo huu uliweza kumuweka kwenye 'levo' za juu barani Afrika.
Akikumbuka lile baridi lazima anyooshe miguu na kucheka kwa furaha.
8.NITAMPATA WAPI
Ni kati ya nyimbo kubwa zilizoweza kumpatia tunzo nyingi za muziki ndani na nje ya Tanzania.Mashairi yake mazuri ,melody kali na video ya kuvutia viliufanya wimbo huu kuwa moja ya nyimbo nzuri barani Afrika ambapo licha ya tunzo ulikuwa ukimpa michongo mingi ya matamasha.
Kweli kwake tatizo halikuwa nyota.
9.NANA
Nana ni wimbo ambao kikawaida tulitegemea ungekuwa ukishindania tunzo mwaka huu lakini mara tuu ulipotoka ulianza kuzoa tunzo nyingi za nje ya nchi.Nana ni moja kati ya nyimbo ambazo huenda alipozitoa hakutegemea makubwa sana lakini wimbo huu umevunja rekodi nyingi ambazo zitamfanya asiusahau.
10.MAKE ME SING
Ulikuwa kama wa kawaida alipoutoa lakini ghafla ukaeleweka na sasa ni moto wa kuotea mbali.Ni wimbo mkubwa si Afrika tuu bali hata alipofanya matamasha nje ya Afrika wimbo huu ulioneke]ana kuwavutia wengi, naamini utakuja kushinda tunzo nyingi za muziki ndani na nje ya Afrika.
Hawezi kuusahau kwani ni motoooo.
Kuna nyimbo nyingi ambazo Diamond Plutnumz hatozisahau lakini hizi ni baadhi ya nyimbo ninazoaminin kutokana na kuwa na historia na mafanikio mbalimbali zitabaki kichwani mwa mtunzi daima.Kumbuka haya ni maoni na mtazamo wangu na si maoni yake na huenda tukatofautiana kabisa nimejaribu tuu kubashiri kwa kusoma matukio na nyakati.
Je, we unaonaje mwanakalamu?
Ungependa nimwandike nani safari ijayo?
Share na wenzako ifike mbali.

UKIWA NA VIPAJI HIVI BONGO TAFUTA MBADALA


Na.Mwanakalamu
Unamsikia Diamond Plutnumz? ni tajiri sijui milionea sijui bilionea lakini ni tajiri, unamfahamu Mbwana Samatta yule aliyekuwa mfungaji bora wa Afrika naye ni tajiri wa kutupwa lakini nadhani wamfahamu Joti yule wa Ze komedi naye ni tajiri na maarufu pia.
Hao wote niliowataja ni baadhi ya watu waliofanikiwa kwa kutumia juhudi na vipaji vyao , swali linakuja;
Je, ni wao pekee wenye vipaji?
Bila kumung'unya maneno kuna wengi sana wenye vipaji tena vya hali ya juu , mara ngapi kijijini ama mtaani kwako unamwona mtu anacheza mpira kwa kiwango cha juu tena kwenye viwanja vibovu mipira ya ovyo chini ya usimamizi wake (yaani bila kocha)?
Mara nagpi unawaona watu wakiwa na vipaji vya kuchora tena bila hata kufundishwa wanachora picha za kuuzwa ndani na nje lakini wanaiishia kuchora vibao vya shule za msingi na sekondari kwa malipo kiduchu tena bila kutambuliwa. Kwenye kuchora nina ushahidi kuna mtu anaitwa Yohana Yohana Haule huyu ndugu ni hatari anachora kweli lakini muulize anajivunia kuwa mchoraji? utakuwa unamuumiza tuu kwani hakuna cha maana cha kujivunia kwa kipaji chake.
Kuna waimbaji wangapi mtaani kwenu ama wachezaji muziki wangapi wa kariba za kina Moze yobo anayelamba pesa za Almas kwa miaka sasa? Wapo wengi lakini wataonekanaje, hakuna namna inapelekea Diamond leo akitaka mrithi wa Yobo atavuka na kwende Nairobi ama Kinshasha kwani huyo mkali wenu atabaki kucheza mtaani ama kuonekana muhuni tuu.
Kuna watu wangapi umewaona ni mafundi kompyuta ,simu, pikipiki, televisheni , redio na magari tena bila kupitia shule ? umewahi kujiuliza watu hao wangeliona darasa je? si wangekuwa wanashindana Maabara wakihangaika kuvumbua teknolojia ya kuifanya nchi yetu kuwa ya kisayansi?
Hakuna kitu.
Sitaki kukumbusha wale rafiki zako mabingwa wa mpira wa kikapu, wavu na mabingwa wa riadha na kuogelea kwani utasikitika tuu wameishia kuwa walevi na mama walizeeka baada ya kufeli darasani huku vipaji vyao vikiwa si bidhaa ya kumfanya tajiri kama Diamond.
Wala sitaki kuwakumbusha wale wachekeshaji waliokuwa wakiwachekesha darasani leo wapo tuu nyumbani hawana hata hela ya chumvi wanamwangalia joti kwenye televisheni za majirani zao ama kwenye mabango barabarani.
Sitaki kabisa kukumbusha wale ndugu zetu waliokuwa wakiigiza sauti za walimu ama hata za walevi barabarani na kutufanya tusiamini kama kweli inawezekana kufanya hivyo.
Unataka nikuulize Moringe ana utajiri ama umaaruufu nje ya facebook licha ya kuwa na uwezo wa kuandika kitu ambacho kitakufanya ujiulize aliwaza nini kabla ya kuandika.
Hii ndiyo Afrika ambayo elimu ni yale ya kwenye mtaala pekee na kufeli mtihani wa darasani basi ni umbumbumbu , ingawa inawezekana kabisa kipaji kikawa mtaji.
TUFANYE NINI.
Natamani kuona tukifanya kitu kwa kizazi tulichopo, nakuomba rafiki yangu niadikie mtu unayeamini ana kipaji kama yupo facebook itapendeza andika jina na kipaji(uwezo) wake kisha tuwaunganishe watu wa makundi hayo waunde umoja na kujadili namna bora ya kuvitumia vipaji vyao.
Mfano wachoraji wajuane hapa na kuunda umoja wao ambao utawafanya wajue namna ya 'kutoka' na wale waliofanikiwa wawaeleze wenzao jinsi ya kunufaika na vipaji vyao wale wachekeshaji pia, waandishi, mafundi na wengineo hivyo hivyo.
TUFANYE HIVYO KWA FAIDA YETU NA TAIFA.
Share ujumbe ufike mbali.

Sunday, 10 April 2016

YUKO WAPI SHETTA AMA SHIKOROBO ISHAMLIPA?



Na.Mwanakalamu

Nilianza kumsikia kwenye nimechokwa akiwa na Belle nine kabla ya kuanza kuporomosha ngoma zilizokuwa kali kama Nidanganye, kerewa, na kuzikamata fikra za wapenda burudani na hata wasiopenda burudani hadi pale alipotoa ngoma iliyotikisa Afrika na mkali kutoka Nigeria KCEE Shikorobo ambayo kwa maelezo yake na hisia za wachunguzi wa mambo ilionekana kumpa madili mengi.

YAJUE HAYA KUHUSU MILIMA

Na.Steven Mwakyusa

Ukiitazama sura ya dunia hasa nchi kavu utakutana na milima na mabonde, ipo milima ya aina mbalimbali kutokana na namna ilivyofanyika mpaka kufikia hapo ilipo!! Milima ni miinuko ambayo ina urefu kuanzia mita 600 toka usawa wa bahari!
#1 Milima iliyopo pwani ya Norway, Brazili, Australia, magharibi mwa India na kwingineko inakadiriwa kuwa na umri wa miaka 1000 mpaka 1200 million!
#2 Kuna aina kuu tatu za milima, milima ya volcano(volcanic mountains), milima mikunjo(fold mountains) na milima tofali(block mountains).
#3 Mlima Everest ndiyo mlima mrefu zaidi katika uso wa dunia kwa maana ya nchi kavu ukiwa na futi 29,028.Mlima Everest unapatikana katika mpaka wa Nepal na Tibet barani Asia!
#4 Mlima Kilimanjaro ni wa 10 kwa urefu duniani ukiwa na futi 19,317.
#5 Milima imekuwa chanzo cha kufanyika mvua kwa kulazimisha upepo wenye mvuke kupanda juu na baadaye kusababisha mvua nyingi katika upande unaopakana na bahari (Windward side), huku upande wa pili ( Leeward side ukipata mvua chache au kukosa kabisa.
#6 Safu ndefu zaidi za milima katika nchi kavu ni milima ya Andes yenye urefu unaofikia 7200 km, katika safu ndefu zaidi ni zile za Mid-Antlantic ridge zenye urefu wa 11,300 km.
#7 Mpaka mwaka 2011 iliaminika kuwa mlima mrefu katika mfumo wa jua ni mlima Olympus mons katika sayari ya Mars wenye urefu wa 21.9 km.
#8 Mlima Rheasilvia unaopatikana katika Vesta Astroid una urefu wa 23km ndiyo mlima mrefu zaidi mpaka sasa katika mfumo wa jua (solar system)
#9 Pamoja na kutokea kwa mmomonyoko wa udongo (soil erosion) unaosababisha na mvua na upepo milima imekuwa ikipungua kwa kiasi kidogo sana, kuna wanasayansi wanaoamini katika kinachoitwa "Isostacy theory"

Saturday, 9 April 2016

YAJUE HAYA KUHUSU UCHAFUZI WA MAZINGIRA

Na.Steven Mwakyusa
Uchafuzi wa mazingira umekuwa ukikua siku hadi siku kutokana na ongezeko la watu duniani likienda sambamba na kuongezeka kwa shughuli za kibinadamu! Kuongezeka kwa uhitaji wa makazi, kukua kwa technolojia hasa uzalishaji katika viwanda, usafirishaji na kilimo vinatajwa kuwa sababu za kuongezeka kwa huu uchafuzi!
Uchafuzi wa mazingira umegawanywa kulingana na kitu kinachoathiriwa moja kwa moja, hapa tuna ardhi(land pollution), hewa(air pollution), maji (water pollution ) na kwengineko zinatajwa kelele(noise pollution)
Athari za uchafuzi wa mazingira zimekuwa kubwa, hasa kwa kusababisha magonjwa na kuua mimea pamoja na viumbe wa majini samaki wakiwemo. Joto limekuwa likiongezeka duniani (global warming ) na kusababisha mabadiliko makubwa ya hali ya hewa!!
‪#‎1 Mto‬ Ganges uliopo India unatajwa kuwa ndiyo mto uliothiriwa kwa kiasi kikubwa na "water pollution"
#2 Inakadiriwa kuwa watoto 1000 wanakufa kila siku nchini India kutokana na magonjwa yanatokana na uchafuzi wa maji.
#3 Kutokana na takwimu la Shirika la Afya Duniani (WHO), katika mji wa Mexico City watu 6400 wanakufa kila mwaka huku wengine zaidi ya 100,000 wakipata matatizo katika mfumo wa upumuaji kutokana na uchafuzi wa hewa(Air pollution)
#4 Kati ya mwaka 1956 na 1968 viwanda nchini Japani vilitupa madini ya Mercury moja kwa baharini, Mercury iliathiri samaki na baadaye mpaka walaji wa samaki na kupelekea watu wengi kuugua na wengine kufa!
#5 BMWs yanatajwa kuwa magari rafiki kwa mazingira huku Mitsubishi na Chyrister yakitajwa kuwa na uchafuzi zaidi wa mazingira. Ila kadri siku zinavyoenda ndivyo magari yanavyozidi kuboreshwa na kutoa moshi kidogo!!
#6 Inakadiriwa zaidi ya computer 130,000 zinatupwa kila siku wakati simu 100 million zinatupwa kila mwaka na kusababisha uchafuzi mkubwa.
#7 Viwanda nchini Marekani vinazalisha kemikali za sumu zinazofikia tani million 3 kila mwaka!

NB; Ukiliangalia suala la uchafuzi wa mazingira "locally" unaweza usione athari zake kwa haraka, ila kama utalitazama "globally", hatari iliyo mbeleni ni kubwa kuliko wengi tunavyifikiri. Japo kufuta kabisa huu uchafuzi ni jambo lisilowezekana, ni wajibu wa kila mmoja kujitahidi kulipunguza hili tatizo. Matumizi ya nishati mbadala kama gesi na solar badala ya mkaa na kuni yanasaidia kupunguza kiwango cha CO2 hewani, pia matumizi ya mboji badala ya mbolea za viwandani inasaidia hata pia kufanya "recycling" ya taka ngumu hasa za plastic!!

YAJUE HAYA KUHUSU KILIMO CHA GREENHOUSE

Na.Steven Mwakyusa
Hiki ni kilimo ambacho kinamuwezesha mkulima kudhibiti mazingira yake kwa maana ya nishati ya jua, unyevu na upepo.
Wazo la kuzalisha mazao katika controlled environment lilikuwepo toka enzi za utawala wa Rumi na baadaye Green zilianza kuundwa na kufanya kazi karne ya 13 huko nchini Italia. Greenhouse imekuwa technolojia inayotumika katika nchi nyingi kuanzia Ulaya mpaka Asia, kumekuwa na project nyingi sana za Greenhouse na zimeonesha kuleta tija kubwa kwa wakulima.
Greenhouse inamuwezesha mkulima kulima mazao hasa ya matunda na mboga. Greenhouse inamuwezesha mkulima kulima katika kipindi chote cha mwaka pasipo kujali misimu.
Ikumbukwe kuwa unaweza kuzuia magonjwa pia wadudu ambao ni hatari kwa mazao. Hili limeonekana kuwa na tija jwa magonjwa na wadudu ni changamoto kubwa katika kilimo ukiachilia mbali mabadiliko yasiyotabirika ya hali ya hewa.
Kabla ya kuamua kujenga Greenhouse unatakiwa kufanya utafiti katika udongo(soil pH, structure, texture &profile) ili ujue kipi cha kuongeza ama kupunguza. Pia unatakiwa kuchunguza aina ya maji na chemikali zilizomo ndani yake.
Kwa Tanzania bado inaonekana ni technologia mpya ila imekuwepo kwa muda sasa. Ukubwa wa Greenhouse unategemea na mahitaji yako pia mtaji ulionao. Kwa mfano material ya kujenga greenhouse y enye ukubwa wa 8m*15m hayazidi 3million, kwa ukubwa huu unaweza kuzalisha mpaka tan 30 za nyanya kwa mwaka na pia Greenhouse ina Guarantee ya kukaa miaka 10.

Friday, 8 April 2016

ROMA USIHANGAIKIE 'TRACE' BADO TUNAKUHITAJI


Na.Moringe Jonasy
Nimekaa sebuleni nikipumzika baada ya shughuli za asubuhi ambazo zinanifanya nihitaji pumziko la nafsi na akili kwani tangu asubuhi nimeichosha sana akili kutokana na kazi ngumu ya kuandaa miswada mitatu ya mashairi,riwaya na tamthiliya ambazo ipo kwenye hatua za mwisho kabla ya kuchapwa.
Siku nyingine muda kama huu ningekuwa juu ya baiskeli nikizunguka huku na huko kukuza ujuzi wa mazingira na tamaduni kwa lengo la kukuza upeo wangu na kujaza maktaba ya kichwa.Leo nimeshindwa kwenda nilikopanga kwenda (KIA) Kutokana na mvua iliyonyesha hivyo nimeamua kukaa na kuanza kusikikiza muziki.
Naam Belle nine alishautaja umuhimu wa muziki akiuweka kama moja ya vitamin ambazo tunazihitaji nami sipuuzi ushauri wake naanza kusikiliza wimbo wake,unafuata wa Samir Nakuombea hapo najikuta nashindwa kusahau mikasa ya mapenzi niliyoshuhudia maishani mwangu baadaye nashindwa kusikiliza wimbo wa Christian Bella 'Nashindwa' kwani naye ananifanya niumie baada ya wimbo huo kugusia maisha yangu ya mahusiano na kuniumiza.
Nakutana na wimbo wa mwana ulioimbwa na Ally Kiba hapo nakumbuka mengi yanayoendela nchini unapoisha wimbo wa nusu nusu unasikika kwenye spika za redio yangu na kuniburudisha haswaa kisha sauti ya bonta inafuata akiimba wimbo wa kura yangu najikuta naurudishia zaidi ya mara tano kabla ya kuendelea ninapokutana wimbo wa ROMA mkatoliki Tanzania.
Hapo nasita kuendelea kusikiliza nyimbo nyingine naufanya huo wimbo uendelee kujirudia kusikika.
Napelekwa mbali kifikra baada ya kusikiliza nyimbo za mwanamuziki huyu ambaye si tuu anajua kuimba bali anajua nini cha kuimba, wakati gani na kwa watu gani.
Je, kuna siku wimbo wa ROMA utapigwa kwenye vituo vikubwa vya redio duniani ama hata Afrika?
Video zake zinaweza kushindania tunzo kubwa za kimataifa?
Nani anamsikiliza ROMA nje ya Tanzania ama Afrika mashariki?
Ni baadhi ya maswali machache yaliyonifanya niyatafutie majibu.
Kwenye suala ya kusikika kimataifa ni jambo gumu labda akianza kuongelea matatizo si tuu ya ndani ya nchi bali ajaribu kuyaongelea ya duniani kwote ama haya Afrika tuu kwani yanafanana kwa kiasi kikubwa, kama rushwa popote ipo, kama ukimwi na imani potofu zipo sehemu nyingi sana ,umasikini usiseme ,uvivu na ukoloni wa weusi wenzetu barani Afrika bado janga kubwa.
Je, kwa kufanya hivyo atasikilizwa Nigeria ama Ghana ambako tangu kizazi cha wapigania uhuru kipite hawajakisikia kiswahili hadi juzijuzi walipoanza kumsikiliza Diamond?
Diamond aliwezaje? Kuwashirikisha na kutoa video zenye ubora.
Je akifanya hayo atasikilizwa ama kutambulika kimataifa?
Hilo bado gumu sana kwani hata sisi hatuwasikilizi wanamuziki wa aina hiyo wanaoimba huko kwao zaidi ya kusikiliza muziki wa aina nyingine na si auimbao ROMA.
Baada ya kujiuliza mwaswali mengi najikuta nikihitimisha kuwa licha ya ROMA kuimba nyimbo zinazohitajika sana kwenye nchi za bara hili lakini bado ana kazi kubwa ya kufika huko akina shetta na Ommy Dimpoz wamefika hivyo namwomba asihangaikie kupigwa trace ama MTV bali aendelee kuhudumia jamii ya kitanzania ambayo naamini bado inahitaji sana elimu aitoayo.
''ROMA tafadhari usihadaike na mafanikio ya wengine binafsi bali endelea kuusaidia unma ufanikiwe"
Naomba kuwaasilisha
Niambie mtazamo wako#mwanakalamumwenzangu

IKO WAPI ZOUK YA BONGOFLEVA?

Na.Steven Mwakyusa
Kuna kipindi katika Bongo flava, ilitokea muziki aina ya Zouk ulipata maarufu na kupendwa na tulio wengi!!
Kwa kifupi Zouk ni mziki mtamu, unasikilizika, unaeleweka na unabeba hisia za kutosha!
Wasanii wakubwa na wachanga walijitahidi kuimba aina hii ya muziki kadri walivyoweza!! Ukitaja manguri basi utaacha kumtaja Mr Paul na vibao vyake kama Zuwena na Harusi, Stara Thomas naye alisikika na vibao kama Mimi na wewe pia Wasiwasi wa mapenzi!!
K bazil pia alifanya vizuri na kibao chake cha Riziki alichoimba na Stara Thomas pia Bizman!! Pia Bizman ambaye alikuwa na mtayarishaji wa muziki katika studio za Soundcrafts hakubaki nyuma, vibao kama Ametoroshwa, nilishe nikulishe, pia Nipe muda vilikonga nyoyo za wengi, Banana Zorro ni mmoja pia ya wasanii waliyoiimba Zouk, huku vibao kama Wasiwasi, mapenzi gani vikimpa chart ya juu!!
Wanaoitwa underground pia walifurukuta kutaka kutoka na aina hii ya muziki, hapa tulimsikia Voice Wonder na Nimpende nani, Hama Q alisikika na Lady, Presssure ya Hafsa Kazinja pia ilimfanya ajulikane, Deo Mwanambilimbi pia hakubaki nyuma, yeye alisikika akiwa na Banana Zorro katika wimbo ulioitwa kwanini!!
Muda ulienda huu muziki ukapotea, na imebaki historia....kipi kiliupoteza hata mimi sijui!!

Thursday, 7 April 2016

HUYU NDIYE 'KID BOY' NINAYEMTAKA

Na;Mwanakalamu
Kwa wadau wa Bongo fleva miaka ya 2000 hakuna ambaye hakumfahamu kijana huyu aliyewavutia wengi kuwa watangazaji wa redio.Anaitwa Sandu George Mpanda maarufu kwa jina la Kid Boy , ni mtangazaji hodari akiwa mmoja wa ule 'utatu mtakatifu' wa Kipindi cha Show Time akiungana na Dj John na Mtoto wa mama Sabuni Glorie Robinson Sabuni, kilikuwa ni bonge la kipindi.Hawakuwa moja wa wale watangazaji wa ''Kitu flani ameizing' hawa walikuwa wakitangaza kwa kiswahili safi siwezi kusema sanifu kutokana na utata wa neno lenyewe usanifu lakini kilikuwa ni kiswahili rasmi.
Kid pia alikuwa mtayarishaji wa muziki pia msimamizi wa wanamuziki , Husein Machozi, Sagna, Baraka Da Prince ,C sir Madini na wengine wengi wamepitia kwenye mikono yake ama akiwa mtayarishaji wa nyimbo zao au hata kuwasimamia lakini kama sikosei alikuwa akihusika kwa kiwango kikubwa katika kuandaa matamasha makubwa ya muziki yaliyokuwa yakifanyika Jijini Mwanza.
Unaikumbuka ''Maneno'' ya Mheshimiwa Temba? Kidboy alihusika katika kuitia kachumbali.
Septemba 2010 nadhani ni mwaka mbaya kwake kama ilivyokuwa kwa mashabiki wake pale alipokutana na janga lililomsababishaia maumivu na hofu kwetu ambao hatukuwa tukibanduka redioni kujua hali yake.Nakumbuka kipindi hicho nikuwa shuleni licha ya kuwa tulikuwa tukizuiwa kuwa na redio kwangu niliona ni makosa kukaa bila kujua hali yake si kwa kuwa alikuwa akinifahamu bali kwa sababu ya uhodari wake katika kutangaza na kuuchambua muziki wa bongo fleva.
Miaka kadhaa baadaye nikashangaa kutomsikia tena redioni hadi pale nipohangaika kutafuta taarifa mtandaoni , nilipokutana na kile kilichoitwa 'tone redio' redio iliyopatikana online na kuambiwa kuwa alikuwa mmoja wa waanzilishi na watangazaji wa redio hiyo ambayo sikupata kuisikia kutokana na kuwa mbali na intanet hadi pale nilipomsikia kwenye Milazo 101 ya Radio one kisha kumwona Bongo 5 hapo nilifarijika kuwa huenda ningemsikia kwa utamu zaidi ama kusoma ule uchambuzi wake ambao daima nilikuwa nikiusikia wakati akitangaza lakini kwa bahati mbaya nilimsikia na kumwona mara mbili siku ya Zari white part pale Mlimani City akimhoji Mwana Fa na Millard Ayo ambaye kwa maneno yake niliona kabisa kumkubali Kidboy na huenda alikuwa mmoja wa watu walimvutia kwenye utangazaji.
Pia nilimsikia kwenye tunzo za watu , tangu hapo nimeishia kulisoma jina lake Bongo 5 akiweka taarifa huku kazi ya kuandika makala za kitafiti na kiuchambuzi zikibaki kuwa kazi ya Fredrick Bundala gwiji mwingine katika utangazaji na uandishi wa kazi za kiuchambuzi na kiutafiti ambaye walau nimekuwa nikimsikia kwenye Chill na Sky.
Leo wakati napitia kwenye ukurasa wa Fredrick Bundala nikakutana na taarifa iliyonivutia na kunifanya nifarijike haswaa!
Kidboy kuwa mkuu wa vipindi kwenye redio mpya LakefmMwanza nikajua zile zama za utangazaji safi zinarudi akiwa kama mwandishi na mtangazaji ule ubora katika tasnia hiyo unategemewa kurudi.
Si tuu katika utangazaji pia kwa upande wa muziki nayaona mabadiliko na maendeleo kwani sina shaka katika kuusema ukweli kuhusu muziki haijalishi mwanamuziki anapendwa ama ni mkubwa lakini anapokosea wimbo fulani ama kitu fulani kwenye wimbo lazima arekebishe mradi apewe nafasi ama aipate nafasi na isipopatikana alikuwa akiitafuta.
Kumbuka kipindi alipokataa kupiga copy za nyimbo za wanamuziki kama vile Kafara ya Tanzanite akiyekopi mbagala ya Diamond Platnumz.
Huyu ndiye Kidboy ninayemtaka najua ataleta mabadiliko na maendeleo katika tasnia ya burudani na habari kwa ujumla.

Naomba kuwasilisha....

Monday, 4 April 2016

LA MADANSA NA KISA CHA KIATU KIPYA


Na.Mwanakalamu
Natumai kila mtu aliwahi kuwa mtoto, na kwenye utoto kuna vituko vyake vya kuaibisha, kuchekesha , vya kujivunia na vya kujifunza pia.Kuna kisa niliwahi kusimuliwa na mama yangu kuwa kipindi hicho nikiwa mdogo siku moja nilinunuliwa viatu , ilikuwa usiku kama wa saa mbili nikapewa kuvijaribu vilinitosha vizuri sana miguuni na vikanipendeza.Sikutaka kuvivua vile viatu baada ya kuvijaribu , siku iliyofuata ilikuwa ya jumapili hivyo ningevivaa niendapo kanisani lakini kwangu ilikuwa ngumu kuvivua hadi walivyovivua kwa nguvu.
Kisa nilivipenda sana.
Asubuhi mama alivyokuja kuniamsha alikuta nimevivaa, yaani nilikuwa nimelala nikiwa nimevivaa, hakujua nilivivaa muda gani hata mwenye sikumbuki maana nilisimuliwa tuu.
Siku ya jumapili niliwahi kanisani kuliko mtu yeyote nikiwa na viatu vipya huku wakati 'Sunday School' inaendelea nilikuwa nikiweka viatu juu ya mabenchi ya kanisani ili wavione hayo mama alisimuliwa na mwalimu wetu wa Sunday school ambaye alikuwa jirani yetu lakini mbaya zaidi nilitamani niingie na viatu hadi bafuni.
Tuachane na kisa hicho hapo juu kuna kitu kimeibuka kwenye muziki wetu wa hapa nyumbani, bongofleva.Kila mwanamuziki ana wacheza shoo wake maarufu kama madansa, hawa kazi yao ni kutumbuiza mwanamuziki akiwa jukwaani huku wakiifanya hadhira iburudike mara dufu.
Akipanda Diamond, na madansa wake wakicheza ndogo mdogo utapenda, Vanessa naye akicheza Closer yake weh! hadi raha Alikiba naye akija na mwana basi wee watu oyeeee!
Kero pale Diamnd akiimba lala salama huku madansa wake wakinyonga nyonga na kucheza kwa staili walizobuni, hapo unaweza jutia hela yako ama Alikiba akiimba Mapenzi yana run dunia huku wale jamaa wakijikunja kunja unaweza tema mate kabisaaa.
Tusishangae Ditto na yeye akaja kuimba Wapo na madansa wakijipinda kufuata muziki wake Duh! kama enzi zangu nalala nimevaa kiatu.
Hili halihitaji kwenda Bagamoyo kuujua muziki ama kuwa na DSTV nyumbani kujua nini cha kufanya bali fikra nusu ya punje ya haradani huweza kutuonesha cha kufanya kuliko kufanya kama mie nilivyojitesa kwa kulala na viatu.
Nyimbo kama lala salama, mapenzi , kamwambie na hata wife wa dunia ambayo kidogo Ally amejitahidi huimba mwenyewe, hizo ni nyimbo za kuwaimbia wanawake hapo ndo utakuta mwanamke anazimia kwa hizia hapo ndipo fleva wa Nigeria huwafanya wadada watamani hata kumgusa na wakimgusa hutokwa na chozi la furaha lile chozi la kumfariji mwanamuziki kwa anagusa mioyo ya watu na si kuturusha watu jukwaani huku ukiimba Cinderela, Sophia ama Mbagala .
Eboh! hilo nalo Jeep.