ads

Monday, 16 February 2026

Darasa anapotupa 'darasa'


 


/Unastruggle for so long (ingawa life is harder)
Everything goes wrong (Ooh)
Hold on and be strong (harder)/
Ndivyo bwana Shariff Thabit Ramadhan alivyoufungua wimbo ambao kwa kijana mtafutaji kwenye nchi ya 'dunia ya tatu' ni kama pambio la kufungia sala yake ya asubuhi kila siku.
Darasa anaanza somo lake akikutaka utembee uone namna dunia ilivyobeba mambo mengi, kuanzia namna tunavyotamani vitu vizuri lakini tunakubali kuwa tutavipata kwa kuvitafuta siyo kuigiza maisha.
Anamwangalia baki bencha na kumweleza kuwa kwao majirani hugombana lakini kwake muuaji huuawa.
Kuna kiherehere wa dawati la mbele anashauri kuhama mtaa.
Darasa anamwambia hawezi kwa kuwa majukumu yamemzidi anaishia kushukuru tu siku ikiisha salama.
Kingine shukuru kumpata 'mtoto' ambaye yupo kumpa moyo mambo yanapokuwa magumu,( ye hajampata mla nauli😁😁)
Kuna sharobaro mmoja anajilamba midomo kabla ya kuropoka 'teacher' ulipigania uhuru tangu zama za TAA ama ulianzisha TANU?
Darasa anakumbuka kuwa alianza kuwalea nduguze katika umri ambao alipaswa kulelewa asikitika tu na kuwakumbuka wana wa mtaa ambao wameozea gerezani kwa makosa ambayo hawakuyatenda.
Anawawaza wategemezi wao ambao wamebaki hawana wa kuwalea.
Kisha kipara cha "monitor " anamkumbusha wana wa mtaa waliotangulia mbele ya haki.
Anamaliza na ;
/Yooh, But life still goes on
Mtaani hakuna dill na roho zipo mkononi
Niggas wanadie kila baada ya nusu saa
Na mademu upondo gani kitaani hawataki kuzaa/
Kengele ya mapumziko inasikika na mzeee wa overrate anaanzisha pambio maarufu la mtaa...
|Even though life is harder life is harder life
Mi sikati tamaa tamaa tamaa
Siku moja ntapataa
Sijali siku nimekosa, nimepata nimekula, nimeshinda njaa
Mi sikati tamaa tamaa tamaa
Siku moja ntapataa|
Je sikati tamaa ya Darasa ni wimbo bora wa Hip hop wa muda wote?

MABIBI NA MABWANA, NAMLETA KWENU CESC FABREGAS




Ukiona watu leo wanapagawa kwa sababu kiungo fulani amepiga pasi mbili tatu za pembeni zilizo safi, ujue wazi hawakuwahi kushuhudia ule upekee halisi, ule ubunifu usiochujwa wa Cesc Fàbregas.
Hapa hatuzungumzii tu mchezaji wa kutengeneza nafasi. Tunazungumzia kijana wa miaka 16 kutoka Barcelona aliyefika Kaskazini mwa London na akaanza kutawala moja ya ligi ngumu na yenye kuhitaji utimamu wa kimwili zaidi duniani.
Yote yalianza pale Arsène Wenger alipoona cheche kwa kijana huyo mdogo, ambaye baadaye aliweka rekodi ya kuwa mchezaji mwenye umri mdogo zaidi kuivaa jezi ya Arsenal wakati huo.
Fàbregas hakuwa tu kinda anayejifunza. Alikuwa jenerali wa uwanjani, akipanga tempo ya mechi kubwa huku wenzake wa rika lake wakiwa bado wanahangaika na mitihani ya shule.
Katika misimu yake nane Arsenal, alicheza mechi 212 za Premier League, akifunga mabao 35 na kutoa pasi za mabao 70 — takwimu za kushangaza kwa mchezaji ambaye hata hajafikisha miaka 25.
Maono yake yalikuwa kama ya kimiujiza. Ndiyo maana aliweka rekodi ya kuwa mchezaji wa haraka zaidi kufikisha pasi za mabao 50 katika historia ya Premier League, rekodi iliyodumu kama alama ya kiwango cha juu kwa miaka kadhaa.
Kilichowafanya mashabiki wa Highbury na baadaye Emirates kumpenda kupindukia ni uwezo wake wa kupenyeza “killer pass” katikati ya mabeki wengi kana kwamba ana jicho la tatu nyuma ya kichwa chake.
Ingawa alitwaa FA Cup moja tu akiwa Arsenal, mchango wake ulikuwa mkubwa kiasi cha kupewa unahodha akiwa na miaka 21 pekee — uthibitisho kwamba uongozi wake ulikuwa wa kiwango sawa na kipaji chake.
Hadithi yake ilipata sura ya kipekee baada ya kurejea Barcelona kisha kurudi tena London, safari hii akiwa amevaa bluu ya Chelsea kutafuta kipande kilichokosekana kwenye safari yake.
Stamford Bridge alithibitisha kwamba ubora hauna mwisho. Alitwaa mataji mawili ya Premier League na katika msimu mmoja akatoa pasi za mabao 18, akikaribia sana rekodi ya muda wote ya msimu mmoja.
Alipomaliza soka lake England, Fàbregas alikuwa amekusanya pasi za mabao 111 za Premier League, akishika nafasi ya pili kwenye orodha ya muda wote, juu ya magwiji wengi waliocheza mechi nyingi zaidi yake.
Historia haisemi uongo. Zile pasi 111 ni ushahidi tosha kwamba Cesc alikuwa mbunifu sahihi na mwenye umakini zaidi kuwahi kucheza kwenye ardhi ya England.
Hakuhitaji kuwa mchezaji mwenye kasi zaidi uwanjani, kwa sababu mpira uliotoka mguuni mwake tayari ulikuwa umefika hatua kumi mbele kabla ya wapinzani kuanza kuukimbiza.
Kutoka yule kijana mwembamba wa Highbury hadi bingwa wa mara kwa mara pale Bridge, safari yake ni tafsiri halisi ya ustadi wa kiufundi.
Hakucheza tu mpira — aliufundisha ulimwengu jinsi ya kuona pengo kati ya mabeki watano ambalo wengine hawakuliona kabisa.
Maestro wa kweli.
Mpangaji wa mchezo wa kiwango cha juu.
Playmaker wa mwisho kabisa.

 

UFUNDI WA MESUIT OZIL


 

Kama wewe ni aina ya shabiki anayevutiwa tu na wachezaji wanaokimbia kama mbwamwitu, basi kwa ukweli kabisa hujafikia kiwango cha kuthamini ule ustaarabu wa kimya na umaridadi wa upasiaji wa Mesut Özil.
Hapa hatuzungumzii kiungo aliyelazimika kupiga kelele au kuingia kwa nguvu kwenye mipira ili kuthibitisha ubora wake; tunazungumzia mtu aliyekuwa anaishi kwenye kiwango kingine kabisa cha uelewa wa mchezo, mchezaji aliyekuwa anaona mianya kwenye safu ya ulinzi kana kwamba ana uwezo wa kusimamisha muda.
Arsenal walipojiandaa kukutana na Wigan katika nusu fainali ile ya 2014 Wembley, ulikuwa mchezo uliobeba uzito wa kumaliza ukame wa miaka tisa bila kombe, na kampeni ambayo Özil alikuwa kichocheo kikuu cha kufufuka kwa Arsenal.
Alipowasili kutoka Real Madrid, hakuwa tu usajili wa kawaida; alikuwa tamko rasmi la dhamira. Alileta hadhi ya bingwa wa Dunia Emirates na kuwa kipande cha mwisho cha fumbo tata la kimkakati la Arsène Wenger.
Takwimu za Özil katika kilele chake ni za kushangaza.
Akiwa Madrid, alikuwa mfalme wa pasi za mabao barani Ulaya kwa misimu mitatu mfululizo — jambo ambalo linasemekana lilimuudhi Cristiano Ronaldo klabu ilipoamua kumuuza mchezaji pekee aliyekuwa anaelewa kila aina ya mbio zake.
Kaskazini mwa London, Özil alivunja rekodi kwa kuwa mchezaji wa haraka zaidi kufikisha pasi 50 za mabao katika Ligi Kuu, na msimu wa 2015/16 alitoa pasi 19 za mabao, akibaki moja tu kufikia rekodi ya kihistoria ya Thierry Henry kwa msimu mmoja.
Hakuhitaji mbio za mita mia kuthibitisha ubora wake, kwa sababu kila mpira uliotoka mguuni kwake ulikuwa na roho yake — uliopimwa kwa ustadi wa hali ya juu kiasi kwamba kazi ngumu zaidi kwenye soka ilionekana kama matembezi ya jioni.
Uzito wa kihisia wa kumtazama Özil ulikuwa kwenye maelezo madogo: pasi zake za “no-look” na ile shuti lake la “bounce” lililowaacha makipa wamesimama kama sanamu huku mpira ukipaa juu yao.
Dhidi ya timu kama Wigan wanaopenda kujilinda kwa “low block” ngumu, Özil alikuwa ufunguo wa mifupa (skeleton key) ulioweza kufungua kufuli yoyote bila jasho wala presha.
Ingawa kuondoka kwake Premier League kulizungukwa na utata, mashabiki wa kweli wa Arsenal hawatasahau usiku ule wa uchawi ambapo alikuwa anaongoza orkesta kwa maono yaliyoonekana kuwa mbele kwa miaka kumi.
Alikuwa taswira halisi ya namba 10 — aina inayopotea katika soka la kisasa linalopenda zaidi nguvu na kazi ngumu kuliko sanaa binafsi.
Özil alitukumbusha kuwa soka, kwa asili yake, ni sanaa — na yeye alikuwa mchoraji bingwa aliyeyaona uzuri katika nafasi tupu ambazo wengine hawakuona chochote.
Alipokuwa na mpira miguuni, uwanja mzima ulikuwa unatulia kwa matarajio, kwa sababu kila mtu alijua kuna jambo la kipekee linakuja — jambo lisilofundishika darasani.
Maestro wa kweli. Jini la kimya kimya.
Mtu aliyekuwa anaona dunia kwa picha ya HD wakati wengine bado walikuwa kwenye rangi nyeusi na nyeupe.

Tuesday, 21 November 2023

BASI













Kaditama nimetua, sisongi sirudi tena,
Mambo nimeyatibua, hata nife hutoguna,
Kweli yote nimejua, ulianza mbali sana,
Basi.
Nilihisi tunaota, kumbe ninajidanganya,
Ilipita myaka sita, sina nililolifanya,
Mwenyewe ukajipata, mwenyewe sikujiponya,
Basi.
Nikaiweka busara, kumbe linaletwa shari,
Kaona kovu imara, kumbe njia ya hatari,
Ninazuia hasira, waniotea kaburi,
Basi.
Kaniundia ubaya, kwote wanone kituko,
Kutwa naijenga kaya, mwenzangu kucha mitoko,
Kila siku kwangu mbaya, kumbe kwako ni ujiko,
Basi.
Kihisi yule adui, kwake utajibagaza,
Nikajifanya sijui, sije wana waumiza,
Nilishajua wewe chui, heri kwangu kunyamaza,
Basi.
Niliposaka suluhu, wapasha vyako viporo,
Kavuka hadi Ruhuhu, Pwani hadi Morogoro,
Kumbe umeshakubuhu, mie kunipa kasoro,
Basi.
Umeutibua moyo, akili na wangu mwili,
Heri un'one na choyo, naipamba yangu hali,
Sasa ninatoka mbiyo, nikusanye zangu mali,
Basi.
Basi sasa imetosha, yote nimeyakubali,
Basi sasa yamekwisha, sasa ninakwenda mbali,
Basi sitokukumbusha, zile ahadi za kweli,

Basi. 

KAMA NINGEKUWA JUA













Huwa halioni wivu, wala kuchukia kitu,
Jua halina uchovu, halibadiliki katu,
Huwa linatunza nguvu, jua si kama msitu,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Jua shahidi wa vingi, wala haliji kusema,
Usiri kwake msingi, halijawahi kugoma,
Iwe mboga iwe bangi, moja hawezi kuchoma,
Heri ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Singetamani usiku, wote mkawa nuruni,
Na nikasirike siku, niwache wiki gizani,
Wacha munone kasuku, mkanitoa thamani,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Mngeona tabasamu, hata nikiwa tabuni,
Mkininyima salamu, isinifike moyoni,
Hata nisiwaze simu, anayepiga ni nani,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Nizipuuze ahadi, mliziweka gizani,
Nisipandishe midadi, mkikana hararani,
Ama kumwona hasidi, akitamba kanisani,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Ugonjwa ningepuuza, na kuikwepa sonona,
Hili linalonunguza, nisingelijali sana,
Kimya ningejiuguza, nikafa hata kupona,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Ningekuwa peke yangu, mwezi na wingu kwa mbali,
Nisingewaza uchungu, nyota siponikubali,
Zaidi ni wangu Mungu, langu pendo astahili,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Singekuwa na wana, nife wakanililia,
Na mke tukagombana, ili aje nikimbia,
Wala kusema hapana, nishindwe kuvumilia,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Nisingemuwaza mama, au baba kumjali,
Huko na huko kusoma, kisha nife kwa ajali,
Mama akashika tama, kuwazia yangu hali,
Kama ningekuwa jua, ningekuwa kitu bora.
Basi hivyo siyo jua, siyo mvua wala nyota,
Macho nitayakodoa, na kusota nitasota,
Nikiumwa naumia, na furaha pia napata,
Kama ningekuwa jua.....

SIKU ZA UJANA WA DIEGO COSTA












Na. Kenny Anjelina

Aliamua kuacha starehe zote za nchini Brazil. Diego Costa the trouble some, akaacha pombe na bata za mitaa ya Rio de Janeiro na Santos.
Akaacha warembo wa fukwe za huko Brazil ambao huzurura na bikini huku wakinywa wine.
Akaicha nchi yake ya Brazil, akaliacha soka murua la samba akanunua uraia wa nchi ya Uhispania. Wahispaniola wakampokea, wakampa jezi namba 19. Wakamuimba kwenye Euro, wakamuimba kwenye Olimpiki, wakamuimba kwenye World Cup.
Mtukutu Diego Costa alikuwa mtu bhana. Wakati akiwa na jezi ya Chelsea na Atletico De Madrid alikuchezea kwanza rafu afu anaweka kwenye kamba. Hakuwa mlaini kama Olmo wa Uhispania ya leo.
Mwaka 2014 Mtukutu Diego Costa alisafiri na timu ya taifa ya Uhispania hadi Brazil kwenye mashindano ya kombe la dunia. Na ndo huko hadithi yangu inaanza.
Uhispania, Chille, Uholanzi na Australia walipangwa kundi 1. Wabrazil wakawa wanaomba Mungu Mtukufu Diego Costa na Hispania yake watolewe kwani wangetukanwa matusi mengi kutoka kwa Costa. Waliogopa kebehi za Costa kutwaa taji kwenye ardhi ya Brazil.
Mechi ya kwanza Spain wakapigwa 5-1 mbele ya Uholanzi. Shukrani kwa Van Persie na the killer Arjen Roben. Mechi ya pili Spain akafa 2-0 mbele ya Chille ya Vidal na Alexis Sanchez.
Hadi hapo Spain wakawa wametolewa. Hadithi ikawa fupi kwa the trouble some Diego Costa.
Wakati anatoka uwanjani wabrazil wakaanza kumzomea huku wakiimba "Adias spana! Adias Amigo!" Yaani kwaheri Rafiki kwaheri mwenzetu. Wabrazil wakanywa pombe na kufurahi usiku ule.

HAPO ZAMANI ZA KALE  

JINSI AMBAVYO RAIOLA ANGEISUMBUA DUNIA KWA MBAPPE












Na. Kenny Anjelina
April 30, 2022 juu ya kitanda kimoja kwenye hospitali ya San Raffaele nchini Italia, Mwanaume mmoja mwenye umri wa miaka 54, alikuwa anavuta pumzi ya mwisho.
Huyu alikuwa ni Mino Raiola, mzee wa fix, mzee wa kuchezesha miamala. Dalali na huni la kimataifa.
Mino Raiola alikuwa wakala wa Haland, Ibrahimovic, Pogba, na wengine wengi. Manchester United hawataki kabisa kumsikia.
Mino alikuwa na nguvu haswa na kazi yake aliifanya kisomi kwelikweli.
Jana, Mbappe amefikisha magoli 300. Nawaza kama Raiola angekuwa hai halafu awe wakala wa Mbappe. Nafikiri vilabu vingi Ulaya vingekaa kwa adabu. Sio PSG siyo Real Madrid, wala Barcelona.
Kwanza angeenda Sky Sports na kusema, "PSG ni timu kubwa, lakini tupo tayari kwa changamoto mpya. Kuna ofa nyingi mezani na tunazifanyia kazi. Lakini kwasasa ni mchezaji wa PSG na anafuraha ".
Hapo PSG wangehaha, kusikia hivyo wangepanga noti nyingi kumshawishi Mbappe aongeze mkataba.
Jumatano, angeenda kwenye gazeti la THE MIRROR na kusema, "Real Madrid ni klabu kubwa na ni ndoto ya kila mchezaji mkubwa. Tunawasikiliza Madrid wanasemaje " Hapo Perez angekunjua noti na kukaa mkao wa kula.
Jumamosi, angeenda THE SUN na kusema, "Jumatatu tutakutana na wawalilishi wa Manchester United kuhusu uhamisho wa Kylian. Ni kijana mdogo ambaye juzi amefikisha magoli 300. Lazima thamani yake iwe kubwa "
Kwahiyo kwa wiki moja tu tayari angewachonganisha PSG, Real Madrid na Manchester United. Ila sasa kumepoa sana.
Haland alitakiwa na Real Madrid wakati akiwa Salzburg. Lakini yeye akampitisha kwenye vituo vingi vya Dortmund na Manchester City ili apige pesa ya udalali mwote humo kabla ya kwenda Madrid au Barcelona. Mino ni Msela haswa.
Kwa vurugu zake na umaarufu wake, angepiga Pauni Milioni 25 pekee yake kwenye dili la Mbappe kwenda Madrid au kwingineko.
Kisha angechukua boti na kwenda kupumzika kwenye fukwe za Venezia akiwa tumbo wazi na mvinyo na warembo pembeni.
RIP RAIOLA

 

KIBURI KINAVYOWAUA WAJERUMANI














Na. Kenny Anjelina

Waingereza wanamsemo wao, Curiosity killed a cat. Yaani udadisi mwingi ulimuua paka. Paka hudadisi hata vitu vinavyomzidi uwezo mwisho hupata madhara na hata kufa.

July 13, 2014, usiku ule Wajerumani walikuwa na furaha sana. Unajua kwanini? Walikuwa wanatwaa taji la Kombe la Dunia, tena njiani wakitoka kutoa semina elekezi kwa Brazil, palepale kwao waliwapa 1-7. Raha iliyoje?

Nafikiri usiku ule pale Rio de Janeiro ndo tulimaliza ubora wa Ujerumani. Tangu hapo hatujaona hata robo ya mafanikio ya ubora wa Ujerumani ile.

Mwaka 2018 waliishia hatua ya makundi pale kwa Vladimir. Walishindwa kufurukuta mbele ya Korea kusini na wahuni Mexico. Bingwa mtetezi, akatolewa hatua ya makundi.

Watu wa mpira walihisi ni bahati mbaya tu. Lakini kilichojirudia mwaka 2022, pale Qatar, kutolewa tena kwenye makundi tukajua tu Ujerumani imeanguka.

Dunia nzima inajua Ujerumani imeisha lakini wao tu pekee ndo hawaamini kama wameisha. Wana kiburi, ndo kinachowaua.

Baada ya Qatar, wakacheza mechi nyingi ambazo zinawapalia kila siku. Lakini hawataki kuanza upya, wanaamini wao bado wapo timamu.

Mpira umebadilika, umetoka kwenye matumizi ya nguvu na kucheza kwa nafasi hadi kwenye matumizi ya sayansi ya mchezo na kutimiza majukumu ya pamoja.

Uingereza, Ufaransa na Uholanzi wapo huko. Argentina ndo tusiseme, unaona jinsi Rodrigo De Paul anavyohaha uwanja mzima. Hakuna matozi tena.

Ila Ujerumani wao bado wanaamini katika nguvu na kupishana. Bahati mbaya wana Gundogan na Musiala ambao hawawezi kutumia mabavu.

Juzi walijaribu kuacha kiburi chao, wakaamua kuiga sayansi kwa kumchezesha Kai Havertz kama mlinzi wa kushoto lakini wakawa wamechelewa, wakafa 3-2 kwa Uturuki.

Ujerumani inabidi wakubali kwamba kizazi cha dhahabu kimeisha, inabidi waanze chini. Kama Uingereza na Uholanzi walivyofanya.

Wakiendelea na udadisi wao watakufa kama ambavyo Italia. Wamekosa michuano miwili ya kombe la Dunia mfulululizo na juzi ilibaki kidogo washindwe kufuzu Euro

DAR NA WATU WAKE










Hawa watu wana nini, kila siku najuliza,
Mkiongea simuni, kweli watakuduwaza,
Ni mabingwa wa kughani, maneno watakujaza,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.

Juzi nilikuwa hapo, sema kazi za ofisi,
Atakweleza alipo, ukija kuna nafasi,
Karibu siye tupo, tena tutajinafasi,
Ile jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Ataleta na matani, atakutoa ushamba,
Jiji utalitamani, kichwani utaliumba,
Jiji lisilo uduni, vile wanavyojigamba,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Mwezi ujao nakuja, utakuwa na nafasi,
Sema lini bwana waja, nipange mambo binafsi,
Tarehe utaitaja, bwana usiwe na wasi,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Kwa kuwa siyo ling'ombe, utapanga na bajeti,
Hutaki maji uombe, au undiwe kamati,
Wajipanga mkatambe, kipato chako cha kati,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Kakangu nipo mjini, nimefika tangu jana,
Ukisha toka kazini,ni vyema tukaonana,
Halafu tukae chini, sizijui nyingi kona,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
E bwana huna habari, ninalo shamba Kimbiji,
Niko bize siyo siri, shamba naliweka mboji,
Vipi utanisubiri, au siyo mkaaji,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Pole sana usijali, ukija tutaonana,
Vipi Kimbiji ni mbali, cha mana jijini sina,
Tutete lile na hili, n'one mnavyopapana,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Wala usihangaike, nikupe namba ya Migi,
Popote akupeleke, kwangu kijana hazugi,
Ni kwa nini uteseke, kuja huku utabugi,
Ila jichanganye wende, utajuta kuzaliwa.
Wawaza Migi ni nani, humjui hakujui,
Heri urudi nyumbani, sije kutana na chui,
Wajipoteza hewani, kisha jijini hukai,
Dar na watu wake, usiende kichwa kichwa.

Thursday, 12 January 2023

WHEN THE STORM COMES


 



 Whether it's a rain storm, 

 I will take off my coat,

 hide you like a tent, 

When the storm comes, I will protect you my love.


I will protect you, dear, 

in words and actions, 

Importantly, I will love you,

When the storm comes, it will not bother you.


It will find me strong, 

and fulfill the duty, 

The duty of a good father, 

A responsible father, 

And a wise husband,

When the storm comes, I will keep you safe. 


I will keep you safe, 

give you the victory, 

The nonsense will stop, 

When the storm comes, I will be your shield. 




I will be your shield, 

you and our children, 

I don't waver here and there, 

betrayal is not a personality, 

When the storm comes, believe that you are safe. 


Believe you are safe, 

safe heart and body, 

You will remain a mother, 

I will not stop working, 

whenever I get a deal, 

When the storm comes, it will find us strong